Saturday, 10 November 2012
MAMBO YA OBAMA NDANI YA OBAMA LAND.
UCHAGUZI wa rais nchini Marekani umemalizika, mgombea wa Democrat, Barack Hussein Obama ameibuka kidedea baada ya kumbwaga wa Republican, Mitt Romney.
Duru za kisiasa nchini humo zinasema kuwa mke wa Rais Obama, Michelle La Vaughn Robinson ni ‘uchawi’ tosha kwa kuwa alichangia ushindi wa mumewe kwa kile kinachotajwa kuwa nyota yake inang’ara ukilinganisha na ilivyokuwa kwa mke wa Romney aitwaye Ann.
Imeelezwa na mitandao mbalimbali kuwa wakati wa kampeni katika majimbo tofauti, Michelle alishangiliwa zaidi na wapiga kura ikilinganishwa na Ann.
Wataalamu wa mambo ya utabiri walisema nguo alizokuwa akivaa Michelle walizozipa jina la election’s purple power dress (nguo za uchaguzi za rangi ya pinki yenye nguvu) zilikuwa zikisaidia kumfanya mumewe, Obama kuwa na mvuto katika uchaguzi huo.
Wachunguzi hao wanasema hasa nguo ya rangi hiyo ya pinki ambayo Michelle alikuwa akipendelea kuivaa, kiutabiri ilikuwa ikiongeza kung’aa kwa nyota ya Obama katika uchaguzi huo.
Hata hivyo, wananchi walikuwa wakisema wazi kuwa mke wa Obama alikuwa anavaa mavazi ya kilalahoi ukilinganisha na zile za Ann na hata siku ya kutangazwa matokeo alivaa ile ya rangi ya pinki.
Michelle aliwashangaza watu katika moja ya midahalo ya wagombea urais ambapo ‘alivunja sheria’ kwa kumzaba kakofi mumewe, kitendo kilichofanya wasikilizaji kumuiga hali iliyomduwaza mwendeshaji wa mdahalo, Candy Crowley.
Aidha, Obama anatajwa kuwa rais anayeongoza Marekani kwa kumpiga mabusu mkewe mara kwa mara tena hadharani.
Suala la nguo liliibuka tena walipokuwa Chuo Kikuu cha Lynn ambapo mavazi aliyovaa Michelle yalikuwa ya kawaida na kushangiliwa na watu hasa wanawake ambao inaaminika kuwa ndiyo waliompa kura nyingi Obama.
Obama baada ya kutangazwa mshindi saa 12:30 Jumatano iliyopita aliingia rasmi tena Ikulu ya White House, jijini Washington DC akiwa amefuatana na mkewe Michelle pamoja na watoto wao Malia (12) na Sasha (9) ambapo wataishi kwa miaka mingine minne.
Labels:
siasa
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment