Friday, 11 January 2013

waziri wa Mifugo Dk. David Mathayo acharuka juu ya uchafu Soko la Samaki Feri


 
…………………………………………………………………………..

WAZIRI wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Dk. David Mathayo, ametishia kuinyaing’anya Halmashauri ya Manispaa Ilala usimamizi wa Soko la Samaki Feri endapo itaendelea kuliacha soko hilo katika hali ya uchafu.
Akizungumza na Fullshangweblog jijini Dar es Salaam jana, Dk. Mathayo alisema wizara yake haiko tayari kuona hali ya uchafu ikiendelea bila ya kupatiwa ufumbuzi.
“Tumekuwa tukiwasisitiza wafanye usafi ili Watanzania waweze kula chakula chenye ubora kwa ajili ya afya zao,” alisema Dk Mathayo.
Alisema halmashauri hiyo bado ina nafasi ya kutafuta mbinu mbadala za kulifanya soko hilo katika hali ya usafi, ili kuepuka hatua zinazokusudiwa  kuchukuliwa na na wizara hiyo.
Hata hivyo, alisema kabla ya kufikia hatua hiyo, wizara itabidi ikutane na Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI).
“Unajua hiki ni kitu cha watu wengi ni lazima kila mtu ahusishwe katika maamuzi yanayoweza kufikiwa na kwa ajili ya maslahi ya wananchi ambao ndiyo wadau wa soko hilo, ” alisema Dk. Mathayo.
Awali, baadhi ya wananchi walieleza kushangazwa kutotekelezwa kwa ahadi iliyotolewa na wizara hiyo kwa zaidi ya miezi sita sasa kuwa endapo halmashauri hiyo itashindwa kudhibiti uchafu, italinyanganya usimamizi.

No comments:

Post a Comment